google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

UZAO WA MASHETANI KATIKATI YA WANADAMU WALIPULIWA KATIKA BONDE LA KUKATA MANENO KAWE.





IBADA YA TAREHE 10-08-2014
SOMO:MASHETANI KATIKATI YA UZAO WA WANADAMU
NA MCHUNGAJI KIONGOZI: JOSEPHAT GWAJIMA


Mchungaji kiongozi Josephat Gwajima

I.                    UTANGULIZI
Asante Mungu kwa ajili ya uwepo wako mahali hapa, Mungu katika jina la Yesu uinuliwe Mungu wetu katika dunia yote kwa maana wewe ni mkuu  kuliko miungu yote, na leo utaenda kujitukuza katikati yetu na kutufunulia yale yote ambayo shetani ameyatenda katika  maisha yetu, leo bwana utaenda kutufunulia uzao wa mashetani  ulioko katikati ya wanadamu na Mungu wetu kwa jina la Yesu utaenda kutufungua na kutuweka huru na uzao wa mashetani.
II.                  SOMO
 Mwanzo 3:15,
15 nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.
 Mungu anatuonyesha kuwa kuna uzao wa aina mbili:-
1.Uzao wa mwanamke – ni wale waliozaliwa na mwanamke kama wewe na mimi,  maana yake wale wanaomfuata Yesu maana Yesu naye ni uzao wa mwanamke.
2.Uzao wa nyoka- wazao wa nyoka ni wale wanaomfuata shetani, Mathayo 23:29-33,
33 Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum?
 Utaona Yesu alipokuwa anaongea na watu wabishi wa neno lake aliwaita nyoka wana wa majoka, Yesu aliwaona kwa ndani kwamba siyo watu ingawa kwa jinsi ya mwili wanaonekana wanadamu kumbe siyo wanadamu ila wamejichanganya katikati ya wanadamu. Leo kwa jina la Yesu tunaenda kuyachambua majoka yote yaliyojichanganya kwa wanadamu , yale yaliyoingia na kuchuchukua nafasi mbalimbali katika tawala za serikali, yale yaliyooa na kuolewa na wanadamu katika jina la Yesu.
Mathayo 3:7, Luka 3:17,Utaona bwana Yesu anawaambia nani aliyewaambia kuikimbia hukumu ya bwana,  Yesu alijua kuwa ni mashetani  ingawa wamevaa miili hivyo  hawaitaji kuokoka kwa maana walishahukumiwa. Leo nakutangazia uzao wa nyoka uliokuletea matatizo katika familia yako, katika biashara yako katika kazi yako leo watang’olewa katika jina la Yesu.
Mathayo 12:34,
34 Enyi wazao wa nyoka, mwawezaje kunena mema, mkiwa wabaya? Maana, kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.
 Bwana Yesu anawaambia nyie majoka mwawezaje  kunena mema kumbe ni waovu, majoka(mashetani) waliovaa miili wanaweza kutenda au kunena mema   ili usiwatambue  kusudi wakuvute na kukupata siyo kwamba wanatenda mema kwako kwa uzuri maana asili ya shetani hawezi kutenda mema.
Mambo matatu muhimu yatakayotokea tunapoekelea katika ulimwengu huu  ni :
1.       Shetani anahama kutoka katika ulimwengu wa roho na kuhamia mwilini kwa kadiri ya Wakristo wanaotumia nguvu za Mungu wanapoongezeka, watu wanaolitumia jina la Yesu wanapoongezeka, ndipo ufalme wa giza unapopigwa sana katika ulimwengu wa roho unabomolewa, hivyo shetani anahamia mwilini  ili kukwepa makombora ya walokole  rohoni yasimpate. Nyakati hizi shetani anaingia katika ulimwengu wa mwili na kufanya biashara , kuoa au kuolewa na wanadamu, lakini leo kwa jina la Yesu tunawafuata mashetani  huko huko mwilini  walipo na kuwang’oa.

2.       Shetani anang’ang’ania  ashikilie tawala za dunia, yaaani wanavaa miili na kuwa viongozi wa serikali katika ngazi mbalimbali duniani kote ili kumtengenezea mpinga kristo njia ili atakapokuja kutawala akute tayari tawala zote zipo chini ya shetani.  Katika jina la Yesu lazima tuwarudishe kuzima walikotoka ili kwanza Tanzania na dunia nzima waokolewe walio wake Yesu ili  watu wa Mungu watakapo kuwa tayari wamenyakuliwa wakati huo mpinga kristo atakapokuja kutawala.Watu wa Mungu nawatangazia kujiingiza kwenye siasa ili wakati wa uchaguzi angalau watu wamchague mwanadamu mwenzao kuliko kuchagua majoka ya aina ya cobra na chatu yaliyovaa miili na kuomba kuchaguliwa katika nafasi mbalimbali.

3.       Wakati mashetani wanahamia mwilini na kuwa binadamu ili wachukue tawala za wanadamu . Mungu naye anafanya mpango wa kuwaleta watu wa mbinguni katika ulimmwengu wa mwili. Malaika wanavaa miili ili kupambana na uovu wa shetani , utaona uamsho usio wa kawaida maana watu wengi wa mbinguni wamevaa miili na kupeleka injili ya Yesu kristo kwa kasi duniani kote. Imeandikwa alitokea mtu ametumwa kutoka kwa Mungu,kumbe Mungu anaweza kumtuma mtu wake na kuitenda kazi ya Mungu, utashangaa unamwona  mtu ananena kwa lugha mpaka cheche zinatoka anafungua watu walioonewa na ibilisi  kwa mamlaka ya jina la Yesu ujue huyo ni mjumbe wa Mungu katikati ya wanadamu.
Maelfu wakiandaliwa katika mpambano na uzao wa mashetani.
Yohana 8:44-45,
44 Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo. 45 Nami, kwa sababu nasema iliyo kweli, hamnisadiki.
 Katika nyakati zinazokuja utaona mapambano makali sana kati ya wale waliovaa miili kutoka kuzimu (mashetani) wakitunishiana misuli na wale waliovaa miili  kutoka mbinguni (wajumbe wa Mungu) ili kwamba dunia nzima waokolewa kabla ya unyakuo wa mwanakondoo  Yesu Kristo.1Yohana3:10, wana wa Mungu ni dhahiri na wana wa ibilisi ni dhahiri pia , wakati huo utaona na kutambua kuwa huyo ni mwakilishi wa Mungu au wa shetani.
Waebrania 2:14, Ibilisi ana nguvu ya mauti, hivyo shetani anapovaa mwili lazima awe wakala wa mauti mbalimbali, mfano mauti ya biashara, mauti ya kazi, mauti ya ndoa . Ndiyo maana utamwona mtu analalamika kuwa biashara yangu iliporomoka nilipoanza kushirikiana na Fulani au ndoa yangu ilivunjika nilipomkaribisha mtu Fulani kwenye nyumba yangu, hii inaonyesha kuwa yule alikuwa wakala wa mauti yaani mjumbe wa ibilisi aliyevaa miili na hii inatufundisha watu wa Mungu kuwa siyo kila mwenye mwili ni mtu lazima unapokutana na mtu lazima uombe kabla ya kushirikiana au kumkaribisha kwako. 
Ezra 9:2,
2 Maana wametwaa binti zao kuwa wake zao, na wake za watoto wao; basi mbegu takatifu wamejichanganya na watu wa nchi hizi; naam, mkono wa wakuu na mashehe umetangulia katika kosa hili.
Mbegu takatifu wamejichanganya na watu wa mataifa, utaona mashetani wanajitahidi kujichanganya na watu ili uzao wa Mungu (mtakatifu) uchafuke na kusudi la Mungu lishindwe kutimia kwa watu wake.

 Katika jina la Yesu mtu yeyote asiye mwanadamu na amejichanganya katika familia yangu, biashara yangu  ndoa yangu na kazi yangu  leo naamuru ayeyuke kwa jina la Yesu.

Namna  shetani aliyevaa mwili anavyoweza kumdhhuru mtu:
1.Anaweza kukurushia matatizo kwa kukwangalia tu. Na wakala wa shetani wanapata nguvu hizo kutoka ama baharini au kwenye mito ambayo ni vituo vya kuongeza nguvu za kishetani.  Zaburi 91:1-5, Yuda 1:6, Ufunuo 12:7, katika maandiko hayo unaweza kuona jinsi shetani anavyoweza kuvaa mwili na kurusha mishale ili kuwadhuru watu wengine. Mtu pia anaweza kurushiwa mishale tangia tumboni na akazaliwa na vifungo ambavyo vinaweza kutesa maisha yake.
 

III. MAOMBI.
Kwa damu ya Yesu baba naomba msamaha kwa jambo lolote nililotenda kwa kujua au bila kujua na likampa shetani nguvu ya kunirushia mishale. Kwa damu ya Yesu bwana Yesu nisamehe na unipe nguvu ya kung’oa mishale yote iliyorushwa kwangu. Kwa jina la Yesu Mungu unipe uwezo wa kumtambua na kumshinda adui yangu shetani aliyevaa mwili na kuishi nami au kushirikiana nami katika maisha yangu.
 Katika jina la Yesu kila mtu  yeyote anayenirushia vitu kwa macho yake au anawarushia watoto wangu au ndugu zangu  naamuru  vimrudie yeye mwenyewe kwa jina la Yesu. kwa jina la Yesu mtu yeyote anayenirushia mishale ya magonjwa, balaa, laana, kushindwa, kuachwa ,mikosi naamuru vimrudie yeye kwa jina la Yesu. katika jina la Yesu naamuru  mishale yote na vitu vyote vilivyorushwa kwangu ving’oke na kumrudia yeye. katika jina la Yesu narudisha mishale yote ya mauti iliyotumwa kwangu iwarudie wao na mimi na watu wangu tutakuwa salama. Na kuanzia leo mwanadamu yeyote aliyevaa mwili kumbe ni shetani nikimwona lazima nimtambue katika jina la Yesu. 
‘’ Imeandikwa nitakuokoa na mshale urukao mchana’’ jina la Yesu naamuru  mishale yote niliyotupiwa   tangia tumboni, mishale ya mauti, mishale ya balaa, naamuru ing’oke katika jina la Yesu. Imeandikwa kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa nami naamuru mishale ya mauti iliyotupwa kwangu ing’oke  kwa jina la Yeskatika jina la yesu nang’oa mishale ya laana ya familia niliyotupiwa tangu tumboni, mishale ya umasikini, mishale ya magonjwa naamuru ng’oka kwa jina la Yesu. Kila mishale iliyotumwa ili nisisonge mbele katika wokovu na maisha yangu naamuru rudi kwa aliyekutuma kwa jina la Yesu.
‘’Imeandikwa  Pinde za mashujaa zimevunjika’’, kwa jina la Yesu navunja pinde zote ambazo mashetani wanatumia kunirushia  mishale magonjwa, balaa, umasikini, kukataliwa, aibu, kwa jina la Yesu naamuru pinde zao zote zivunjike na ghala za mishale yao ziteketee kwa moto kwa jina la Yesu.
‘’Imeandikwa kila pando asilolipanda baba yangu wa mbinguni litang’olewa’’,  leo kwa jina la Yesu nawakamata kwa mikono ya chuma katika ulimwengu wa roho  mashetani wote waliovaa miili Dar es salaam  na kuwang’oa kwenye miili yao warudi kuzimu na miili yao naizika kwa jina la Yesu. Nawafuata mashetani wote waliovaa miili Morogoro nawang’oa na kuwaamuru warudi kwao kuzimu kwa jina la Yesu. Nawanyofoa kwenye miili mashetani wote walioko Mwanza nawamuru kurudi kuzimu na kuachia maisha ya watu wa Mungu kwa jina la Yesu, Nawafuata mashetani wote walioko Kagera ambao wameoa na kuolewa na wanadamu na wamesababisha matatizo kwenye maisha ya watu nawang’oa na kuwaponda vichwa vyao na kuwarudisha kuzimu na miili yao izikwe kwa jina la Yesu. Naikamata Tanzania yote na mikoa yote kila shetani aliyevaa mwili lazima ang’oke na kurudi kuzimu kwa jina la Yesu.
Ameni.

Post a Comment

0 Comments