google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

KWANINI HUKUOGOPA?


JUMAPILI YA TAREHE 28/12/2014
MCHUNGAJI KIONGOZI JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: KWANINI HUKUOGOPA?

“Ikawa baada ya kufa kwake Sauli, hapo Daudi aliporudi katika kuwaua Waamaleki, naye Daudi amekaa siku mbili katika Siklagi; hata siku ya tatu ikawa, tazama! Akaja mtu kutoka kambi ya Sauli, nguo zake zimeraruliwa, tena ana mavumbi kichwani mwake; basi, ikawa alipomfikia Daudi, akaanguka chini, akamsujudia. Daudi akamwambia, Umetoka wapi? Akamwambia, Nimeokoka katika kambi ya Israeli. Daudi akamwambia, Yalikwendaje? Tafadhali uniambie. Akajibu, Watu wamekimbia vitani, tena watu wengi wameanguka wamekufa; hata Sauli naye na Yonathani, mwanawe, wamekufa. Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Umejuaje ya kuwa Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa? Yule kijana aliyempa habari akasema, Nalikuwapo kwa nasibu juu ya kilima cha Gilboa, na tazama, Sauli alikuwa ameegemea fumo lake; na tazama, magari na wapanda farasi wanamfuatia kwa kasi. Naye alipotazama nyuma, akaniona, akaniita. Nikajibu, Mimi hapa. Akaniambia, U nani wewe? Nikamjibu, Mimi ni Mwamaleki. Akaniambia, Tafadhali simama karibu nami, ukaniue, maana shida imenipata; kwa sababu roho yangu ingali hai ndani yangu. Basi, nikasimama karibu naye, nikamwua, kwa sababu nalijua hakika ya kuwa hawezi kupona baada ya kuanguka; kisha nikaitwaa ile taji iliyokuwa kichwani mwake, na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, nami nimevileta hapa kwa bwana wangu. Ndipo Daudi akashika nguo zake akazirarua na kadhalika watu wote waliokuwa pamoja naye; wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga. Naye Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Watoka wapi wewe? Akajibu, Mimi ni mwana wa mgeni, Mwamaleki. Daudi akamwambia, Jinsi gani hukuogopa kuunyosha mkono wako umwangamize masihi wa BWANA? Ndipo Daudi akamwita mmoja wa vijana, akamwambia, Mwendee, ukamwangukie. Basi akampiga hata akafa. Daudi akamwambia, Damu yako na iwe juu ya kichwa chako mwenyewe; maana umejishuhudia nafsi yako ukisema, Nimemwua masihi wa Bwana.” 2 Samweli 1:1-16


Daudi alikuwa mwenye umri wa miaka 16 tu alipomuua Goliathi, naye Mfalme Sauli akapata hisia kwamba huyu kijana kwa nguvu zake anaweza akawa Mfalme badala yake. Hivyo akaanza kumwinda Daudi ili amuue. Hivyo Daudi akawa mtu wa kutangatanga akimikimbia Sauli. Daudi akiwa porini akijificha Sauli akaenda vitani na Wafilisti. Daudi hakuwa sehemu ya vita hii kwa kuwa alikuwa mafichoni.

Baada ya vita kuwa imeisha, Daudi akamuona huyu kijana Mmaleki ambaye alikuja kumjuza taarifa za yaliyojiri vitani. Kijana huyu anaeleza na kusema kuwa Mfalme Sauli pamoja na mwanae Yonathani wameuawa vitani na anakiri kuwa yeye ndiye aliyemuua na kisha anatoa sababu kuwa alijua asingepona mbele ya Wafilisti. Inaonekana kijana Mmaleki alijua kuwa Daudi na Sauli ni maadui hivyo alitegemea Daudi afurahi. Lakini mambo yalikuwa tofauti kidogo. Daudi aliposikia hayo akararua mavazi yake akayatupa chini pamoja na mashujaa wake wakaacha kula mpaka jioni wakiumwombolezea Sauli masihi wa Bwana.
Masihi wa Bwana ni mtu ambaye amepakwa mafuta na Mungu ili atengwe kwa ajili ya kazi ya Bwana. Katika agano la kale watu waliopakwa mafuta ni mfalme, kuhani na nabii. Vilikuwepo vyombo ambavyo vilipakwa mafuta pia kwa ajili ya kazi ya Bwana. Neno masihi ni sawa na neno Kristo yaani aliyetengwa kwa ajili ya Bwana. Ndio maana biblia katika ufunuo inasema kuwa katika siku za mwisho watatokea makristo wa uongo, haisemi maYesu wa uongo.
Kwa desturi za kiyahudi mtu hawezi kuitwa masihi mpaka amwagiwe mafuta maalum na nabii. Hii ndio sababu iliyowafanya wayahudi wamkatae Yesu kwasababu alijiita Kristo “masihi wa Bwana” bila kuwa amepakwa mafuta na nabii yoyote waliyemfahamu wao. Umasihi ni uungu wa Mungu juu ya mwadamu; mwanadamu anakuwa ana vipande viwili uwanadamu wake na uungu ulioko ndani yake.  Katika agano jipya mtu anakuwa masihi wa Bwana si kwa kumwagiwa mafuta tena bali kwa kujazwa Roho Mtakatifu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Yesu, alipokuwa anabatizwa lilishuka wingu zito kutoka juu nah ii ndio ilikuwa ishara kuwa amemwagiwa Roho Mtakatifu. Lakini Wayahudi hawakuelewa mambo haya.

Biblia inasema;

“Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.” Zaburi 105:15

Daudi aliliifahamu jambo hili vizuri. Sio kwamba hakupata nafasi ya kumuua Sauli; lakini mara zote hakufanya hivyo kwa kuwa alijua kuwa pamoja na uovu wote anaomfanyia bado Sauli ni masihi wa Bwana na hapaswi kuguswa.
“Ikawa, Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa ya kwamba, Daudi yuko katika nyika ya Engedi. Ndipo Sauli akatwaa watu elfu waliochaguliwa katika Israeli wote, akaenda kumtafuta Daudi na watu wake juu ya majabali ya mbuzi-mwitu.  Akafika penye mazizi ya kondoo kando ya njia, na huko kulikuwa na pango; Sauli akaingia ndani ili kuifunika miguu. Na Daudi na watu wake walikuwa wakikaa mle pangoni ndani sana. Nao watu wa Daudi wakamwambia, Tazama, hii ndiyo siku ile aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mikononi mwako, nawe utamtenda yo yote utakayoona kuwa mema. Basi Daudi akainuka, akaukata upindo wa vazi lake Sauli kwa siri.  Lakini halafu, moyo wake Daudi ukamchoma, kwa sababu amekata upindo wa vazi lake Sauli. Akawaambia watu wake, Hasha! Nisimtendee bwana wangu, masihi wa BWANA,neon hili,kuunyosha mkono wangu juu yake,kwa maana yeye ni masihi wa BWANA.” 1 Samweli 24:1-6
Daudi akasema, Aishivyo Bwana, Bwana atampiga; au siku yake ya kufa itampata; atashuka kwenda vitani na kupotea. Hasha! Nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi.”1 Samweli 26:10-11

 Hasha! Nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi. Basi Daudi akalitwaa lile fumo, na lile gudulia la maji, kichwani pa Sauli; nao wakaenda zao, wala hapana mtu aliyeliona jambo hili wala kulijua, wala kuamka; maana wote walikuwa wamelala; kwa kuwa usingizi mzito kutoka kwa Bwana umewaangukia.” 1Samweli 28:11
Hizi zote zilikuwa ni nyakati tofauti ambazo Daudi aliweza kumuua Sauli lakini hakufanya hivyo kwa kuwa alijua ni masihi wa Bwana. Na kwa sababu ya hili, Mungu alimpenda sana Daudi. Katika biblia ni watu wawili tu ambao Mungu alitamka waziwazi kuwa alipendezwa nao na Daudi ni mmoja kati ya watu hao mwingine akiwa ni Yesu.
Baada ya kuomboleza kwa ajili ya Sauli na Yonathani, Daudi alimgeukia yule kijana Mmaleki na kumuuliza, “Jinsi gani hukuogopa kuunyosha mkono wako umwangamize masihi wa BWANA?”  Kumbe Mungu anategemea tuwe na hofu kunyoosha mikono na midomo yetu kuwaangamiza masihi wake.
Kisha Daudi aliamuru kijana Mmaleki auawe kwa sababu alikiri kwa nafsi yake kuwa alimuua masihi wa Bwana. Lakini ukweli ni kwamba kijana huyu hakumuua Sauli, alikuta amekwishauawa. Naye kwa kutaka sifa mbele ya Daudi akadanganya na kuishia kuuawa.
Ipo laana itokanayo na wewe kuwaongelea vibaya watumishi wa Mungu. Haijalishi ni watumishi wa kanisa lako au lingine. Ubaya wa laana ni kuwa madhara yake  hayataonekana leo au kwa wakati mmoja. Itakutafuna wewe, familia yako, biashara polepole mpaka vyote vimeisha kabisa. Biblia iinayo mifano ya namna watu walivyobeba laana katika maisha yao kwa kuwainukia masihi wa Bwana kwa maneno au matendo.
“Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi.  Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao.  Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.  Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje.  Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili.Kisha akawaambia,Sikizeni basi maneno yangu;Akiwapo nabii kati yenu,Mimi,Bwana,nitajifunua kwake katika maono,Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake.  Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma.  Kisha Haruni akamwambia Musa, Ee bwana wangu nakusihi sana usituwekee dhambi juu yetu, kwa kuwa tumefanya ya upumbavu, na kufanya dhambi. Nakusihi, asiwe kama mmoja aliyekufa, ambaye nyama ya mwili wake nusu imelika hapo atokapo tumbo la mama yake. Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake. Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma. Kisha Haruni akamwambia Musa, Ee bwana wangu nakusihi sana usituwekee dhambi juu yetu, kwa kuwa tumefanya ya upumbavu, na kufanya dhambi.  Nakusihi, asiwe kama mmoja aliyekufa, ambaye nyama ya mwili wake nusu imelika hapo atokapo tumbo la mama yake. Musa akamlilia Bwana, akasema, Mpoze, Ee Mungu, nakusihi sana. Bwana akamwambia Musa, Je! Kama baba yake angalimtemea mate usoni tu, hangaliona aibu muda wa siku saba? Na afungwe nje ya kambi muda wa siku saba, kisha baada ya hayo ataletwa ndani tena. Basi Miriamu alifungwa nje ya kambi muda wa siku saba; wala watu hawakusafiri hata Miriamu alipoletwa ndani tena. Baada ya hayo watu wakasafiri kutoka Haserothi, wakapanga kambi katika nyika ya Parani.” Hesabu 12:1-16
Miriamu na Haruni walikuwa ndugu wa damu kabisa wa Musa. Miriamu alikuwa ndiye dada mkubwa wa Musa aliyehusika kumficha Musa Farao alipotoa amri ya watoto wa kiume kuuawa katika Misri. Miriamu na Haruni pia walikuwa watumishi wa Mungu; Miriamu akiwa mwimbaji na Haruni kuhani. Kwa hiyo walikuwa wamemzoea sana Musa na wakashindwa kuuona umasihi wake hata wakaanza kumsema juu ya mke aliyemuoa aliyekuwa mkushi yaani mwafrika. Walichosahau kina Miriamu ni kuwa mtu anapochaguliwa kuwa masihi wa Bwana mara moja anabadilika na kuwa si mtu wa kawaida tena kwa kuwa Mungu anakuwa anafanya kazi kupitia yeye. Hii haimaanishi kuwa atakuwa mtakatifu asiyetenda dhambi kabisa, hapana. Anaweza akakosea kabisa kwa sababu ile sehemu ya uanadmu bado imo ndani yake pia. Ni kweli haiikuwa sahihi kwa Musa kuoa mwanamke Mkushi kwa sababu Mungu mwenyewe ndiye aliyeweka sheria hiyo kati ya Waisraeli. Lakini haikuwa sehemu ya kina Miriamu kuhukumu jambo hilo kama ambavyo leo sio nafasi yako kuwahukumu na kuwasema watumishi wa Mungu hata kama wamekosea kweli. Acha Mungu mwenyewe liyewachagua ashughulike nao.  Ni muhimu sana ufahamu kuwa Watu hawawi watumishi wa Mungu kwa sababu wametaka au kwa kuwa wanaweza bali ni kwa sababu wamechaguliwa na Mungu.
Tunaona jinsi laana ya ukoma ilivyompata Miriamu kwa kumsema Musa masihi wa Bwana; Musa hakuwa ameyasikia haya maneno lakini biblia inasema Mungu alisikia. Inawezekana kweli maneno yako unayasemea mbali kabisa na mtumishi husika lakini kumbuka Mungu anasikia. Wakati mwingine unamsema mtumishi wa Mungu vibaya halafu unapofika mbele yake unajifanya kuwa mnyenyekevu naye hutamka baraka juu yako na wewe unaitikia “Amina!”  Zile Baraka hugeuka na kuwa laana katika maisha yako.
Kama ambavyo ilibidi Miriamu atengwe kwa siku saba hata baada ya Musa kumuombea msamaha kwa Bwana; ndivyo inavyokuwa kwenye maisha yetu hata leo. Wakati mwingine safari ya kiroho ya mtu inaweza kukwama kwasababu ya kuwasema watumishi wa Bwana.
“Basi Kora, mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, akatwaa watu, pamoja na Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni, mwana wa Pelethi, waliokuwa wana wa Reubeni;  nao, pamoja na watu kadha wa kadha wa wana wa Israeli, watu mia mbili na hamsini, Wakuu wa mkutano, waliokuwa wateule wa mkutano, watu wenye sifa, wakainuka mbele ya Musa; Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia,  Jitengeni ninyi mkaondoke kati ya mkutano huu, ili nipate kuwaangamiza mara moja.  Nao wakapomoka kifudifudi, wakasema, Ee Mungu, Mungu wa roho za wenye mwili wote, je! Mtu mmoja atafanya dhambi, nawe utaukasirikia mkutano wote? Bwana akasema na Musa, na kumwambia, Nena na mkutano, na kuwaambia, Ondokeni ninyi hapo karibu na maskani ya Kora, na Dathani, na Abiramu. Basi Musa akainuka na kuwaendea Dathani na Abiramu; na wazee wa Israeli wakaandamana naye.  Akasema na mkutano, na kuwaambia, Nawasihi, ondokeni penye hema za hawa watu waovu, wala msiguse kitu chao cho chote, msiangamizwe katika dhambi zao zote.  Basi wakaondoka hapo karibu na maskani ya Kora, na Dathani na Abiramu, pande zote; nao kina Dathani na Abiramu wakatoka nje wakasimama mlangoni mwa hema zao, pamoja na wake zao, na wana wao na watoto wao wadogo. Musa akasema, Kwa jambo hili mtajua ya kwamba Bwana amenituma, ili nifanye kazi hizi zote; kwa kuwa mimi sikuzifanya kwa akili zangu mwenyewe. Kama watu hawa wakifa kifo cha sikuzote, kama watu wote wafavyo, au kama wakipatilizwa kwa mapatilizo ya watu wote; hapo basi Bwana hakunituma mimi.  Lakini Bwana akiumba kitu kipya, na hiyo nchi ikifunua kinywa chake na kuwameza, pamoja na wote walio nao, nao washukia shimoni wali hai; ndipo mtatambua ya kwamba watu hawa wamemdharau Bwana Basi ilikuwa, hapo alipokwisha kusema maneno haya yote, nchi iliyokuwa chini yao ikapasuka; nchi ikafunua kinywa chake, na kuwameza, na watu wa nyumba zao na wote walioshikamana na Kora, na vyombo vyao vyote. Basi wao, na wote waliokuwa nao, wakashukia shimoni wali hai; nayo nchi ikawafunika wakaangamia kutoka mle mkutanoni. Nao Israeli wote waliokuwa kando-kando yao wakakimbia kwa ajili ya kilio chao; kwa kuwa walisema, Nchi isije kutumeza na sisi.  Kisha moto ukatoka kwa Bwana, ukawateketeza hao watu mia mbili hamsini waliofukiza uvumba.” Hesabu 16:1-35
Huu ni mfano mwingine wa watu ambao waliinuka kinyume na mtumishi wa Mungu Musa na laana ya mauti ikawakumba. Si wao tu bali familia zao pia.
Kuna sehemu katika maisha yako sio maombi au kusoma neno au kutoa kwako sadaka kutaweza kukuvusha bali neema tu ya Mungu. Lakini Mungu naye anaweza akakumbuka yale maneno yako mabaya juu ya watumishi wake uliyoyanena naye akanyamaza. Kama ambavyo dhabihu na maombi hukumbukwa mbele za Bwana ndivyo yatakavyokumbukwa maneno yako. Ni kweli Bwana kasema nasi kuwa mwaka 2015 ni mwaka wa kutiisha, kumiliki na kutawala lakini tusipoangalia tutaishia kusema bila kupokea. Kwa nini? Laana ya kuwasema masihi wake.
Kuwasema watumishi wa Mungu au wakuu wa watu wako kunaleta laana iwe ulisema kwa kutokujua au kwa kurubuniwa na watu. Sio lazima itokee leo lakini hakika yake itakupata hata kama ni miaka kumi ijayo. Basi leo kwa kadri ambavyo unahukumiwa ndani yako fanya toba ya kweli. Biblia inasema aziungamaye dhambi zake na kuziacha atasamehewa. Baada ya toba dhamiria kabisa kutoka ndani yako kutokuwasema watumishi wa Mungu wawe wa kanisa lako au lingine. Utakapokutana na mtu au watu ambao wametengeneza kikao cha kuwasema watu wa Mungu hakikisha unawataarifu kuwa si sawa na pia ujitenge nao. Usikubali kuishi ndani ya laana kwa kushindwa kukizuia kinywa chako kusema yasiyostahili.
 
TUTAKUWA NA MFUNGO WA SIKU 30 KUANZIA 1/1/2015 MPAKA 30/1/2015. MFUNGO HUU UTAAMBATANA NA MAOMBI YATAKAYOFANYIKA KUANZIA SAA TISA ALASIRI KATIKA VIWANJA VYA TANGANYIKA PACKERS. PIA, MAOMBI HAYA YATAAMBATANA NA MAFUNDISHO JUU YA SERIKALI YA SHETANI NA MAPEPO YANAYOTAWALA SIKU. KARIBU TUUANZE MWAKA 2015 KWA NGUVU. MFUNGO HUU NI KWA AJILI YA KILA MTU, HIVYO WAKARIBISHE NDUGU, JAMAA NA MARAFIKI ZAKO. HAKITAKUWA KITU RAHISI LAKINI MUNGU AKUTIE NGUVU UWEZE KUFUNGA NA KUHUDHURIA IBADA HIZI ZA MAOMBI NA HAKIKA BAADA YA TAREHE 30/1/2015 UTAKUWA MTU WA OFAUTI KWA JINA LA YESU. KARIBU TUTIISHE, TUMILIKI NA KUTAWALA!

Post a Comment

0 Comments